Serikali ya Mapinduzi Zanzibar

wizara ya Fedha na Mipango

Author name: info@mofzanzibar.go.tz

Uncategorized

NYENZO YA BAJETI YAZINDULIWA

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar, imesema kwa kutambua umuhimu wa jinsia na wazee katika maendeleo ya kijamii kwa mwaka wa fedha 2026/2027 imetenga bilioni 449 katika kutekeleza mpango huo.  Waziri wa Fedha na Mipango Dk. Juma Malik Akil aliyasema hayo wakati akizindua nyenzo za bajeti inayozingatia jinsia (GRV) katika ukumbi wa Wazee Sebleni. Alisema hicho ni kiwango kikubwa ambacho kitawezesha kutekeleza jambo hilo kwa ufanisi kwani bajeti ya mwaka 2025/2026 ilitenga shilingi bilioni 70 pekee. Alifahamisha kuwa uzinduzi huo una umuhimu wa kipekee kwani unafanyika wakati Zanzibar inahitimisha utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Jukwaa la Kizazi Chenye Usawa (Generation Equality Forum) wa miaka mitano, 2021–2026. “Uzinduzi huu ni miongoni mwa mafanikio muhimu ya utekelezaji wa ahadi hizo na unaonesha dhamira ya serikali ya kuimarisha usawa wa kijinsia na uwajibikaji wa matumizi ya rasilimali za umma,” alisema. Alisema bajeti ndio nyenzo kuu ya serikali katika kutekeleza sera na mipango ya maendeleo kwani kupitia bajeti, serikali huamua namna rasilimali zitakavyogawiwa na huduma zitakavyotolewa kwa wananchi. Aidha alisema ni muhimu kuhakikisha kuwa maamuzi hayo yanazingatia mahitaji halisi ya wanawake, wanaume, wavulana  na wasichana ili kuwa na maendeleo jumuishi na yenye manufaa kwa wote. Dk. Malik alisema nyenzo hizo zitachangia utekelezaji wa Dira ya Zanzibar 2050, Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar (ZADEP), Sera ya Jinsia ya Zanzibar ya mwaka 20216 na Mpango wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto awamu ya pili wa mwaka 2025/2026– 2030. Waziri Malik alisisitiza kuwa uzinduzi wa vifaa hivyo si mwisho wa safari, bali ni mwanzo wa hatua mpya ya utekelezaji hivyo alizihimiza wizara, Idara na taasisi za serikali, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Baraza la Wawakilishi, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali na wadau wengine kuhakikisha kuwa vifaa hivyo vinatumika kikamilifu katika majukumu yao ya kila siku Alisema sasa kuna wizara tisa ambazo zinatekeleza mpango huo kwa majaribio na anaamini zitaweza kuongezeka ili kufikia katika kutekelekeza ngazi yote ya kitaifa. Aliipongeza UN Women kwa kuendelea kuwa mshirika muhimu wa serikali katika kuimarisha usawa wa kijinsia, uwezeshaji wa wanawake na kuendeleza utawala bora na maendeleo jumuishi, Umoja wa Ulaya (European Union) na Gates Foundation kwa msaada wao wa kifedha uliowezesha maandalizi, mapitio na ukamilishaji wa vifaa hivyo muhimu. Naye, Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Anna Attanas Poul, alisema uzinduzi huo ni hatua muhimu kwani itaimarisha uwezo wa wizara na wadau wake kuhakikisha kuwa masuala ya kijinsia yanazingatiwa kikamilifu katika mipango, bajeti na utekelezaji wa programu za maendeleo. Alisema alisema UN Women kwa kushirikiana na washirika wake wameendelea kuiunga mkono serikali katika kuimarisha Bajeti Inayozingatia Jinsia na usimamizi wa fedha za umma unaozingatia usawa na ujumuishi. Kwa upande wake Mwakilishi wa UN Women Tanzania, Catharine Gifford, alisema bajeti inayozingatia jinsia ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha rasilimali za umma zinawanufaisha wananchi wote kwa usawa bila kujali jinsia. Aliipongeza SMZ kwa juhudi zake za kuingiza masuala ya kijinsia katika mifumo ya mipango na bajeti kwani bajeti inayozingatia jinsia sio bajeti maalumu kwa wanawake au wanaume pekee bali ni mfumo unaolenga kuhakikisha sera, mipango na matumizi ya fedha za umma yanazingatia mahitaji ya wanawake, wanaume, wasichana na wavulana kwa usawa. Alibainisha kuwa mbinu hiyo husaidia kubaini makundi yanayonufaika na matumizi ya umma na yale yanayoweza kubaki nyuma katika mchakato wa maendeleo. Hivyo, aliahidi kuwa UN Women itaendelea kushirikiana na serikali na wadau mbalimbali ili kuhakikisha masuala ya kijinsia yanaingizwa kikamilifu katika upangaji wa mipango, ugawaji wa bajeti na utoaji wa huduma kwa wananchi wote.

Uncategorized

BAJETI YA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO KUWASILISWA

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Juma Malik Akil, amebainisha vipaumbele tisa vya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/2027, vikiwemo kuimarisha usimamizi wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali, kusimamia utekelezaji wa bajeti inayozingatia usawa wa kijinsia pamoja na kupitia sera, sheria, kanuni na miongozo mbalimbali kwa lengo la kuongeza ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma za Serikali. Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwaka wa fedha 2026/2027 katika kikao cha 30 cha Baraza la Wawakilishi kilichofanyika Chukwani, Dkt. Juma amesema wizara hiyo itaendelea kusimamia nidhamu ya matumizi ya fedha za umma, kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato na kuweka mazingira bora yatakayochochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar. Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati ya bajeti ya Baraza la Wawakilishi, Bakari Hamad Bakar, amesema kamati hiyo inashauri wizara kuhakikisha kunakuwepo na matumizi yenye tija ya fedha za umma ili mipango iliyopangwa iweze kutekelezwa kwa ufanisi na kuleta manufaa kwa wananchi pamoja na kukuza uchumi wa nchi. Wakati huo huo, baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliochangia hotuba hiyo wamesisitiza umuhimu wa kuimarishwa kwa ukusanyaji wa mapato ya ndani, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa wakati ili kufikia malengo yaliyokusudiwa. Akijibu hoja za wajumbe, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Juma Malik Akil, amesema Serikali itaendelea kuyafanyia kazi mapendekezo yote yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa bajeti na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Zanzibar. Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliipitisha bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango ya zaidi ya shilingi trilioni nane kwa ajili ya kutekelezav majukumu na vipaumbele vilivyoainishwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Uncategorized

MAKATIBU WAKUU WAKUTANA KOREA

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar Ndugu Aboud Hasan Mwinyi ameongoza ujumbe wa Tanzania katika kikao cha Makatibu Wakuu wa nchi za Afrika na Korea uliofanyika jijini Seoul nchini Korea. Mkutano huo umefanyika tarehe 1 na 2 Juni, 2026.

Uncategorized

MWENYEKITI WA SUKUK APONGEZA SERIKALI

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Zanzibar Sukuk1 Limited, Juma Amour Mohamed, amempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Ali Mwinyi, kwa maono na juhudi zake za kuanzisha mfumo wa hati fungani za Kiislamu (Sukuk), akisema hatua hiyo ni ya kihistoria katika kuimarisha sekta ya fedha visiwani humo.Akizungumza kuhusu mafanikio ya hatua hiyo, Juma alisema Zanzibar inalenga kuwa kitovu cha huduma za fedha za Kiislamu katika ukanda wa Afrika Mashariki. Alieleza kuwa kuanzishwa kwa hati fungani zinazoendeshwa kwa misingi ya Sharia kumejibu kilio cha muda mrefu cha taasisi za fedha za Kiislamu zilizokuwa zikikosa fursa salama za uwekezaji. Alisema kabla ya kuanzishwa kwa Sukuk, benki na taasisi nyingine za kifedha zilizokuwa zikitoa huduma za Kiislamu zilikuwa zikikabiliwa na changamoto ya ukwasi mkubwa (liquidity) bila kuwa na maeneo yanayokubalika kisheria kwa uwekezaji. Hali hiyo ilisababisha kupungua kwa ufanisi wa utendaji katika soko la fedha. “Benki za Kiislamu zilikuwa na fedha nyingi lakini hazikuwa na miradi au dhamana zinazokidhi matakwa ya Sharia kwa ajili ya kuwekeza. Hii iliathiri utendaji wao na hata kuwanyima watu binafsi fursa za uwekezaji halali,” alisema. Aliongeza kuwa kuanza kwa Sukuk kumesaidia kukamilisha mnyororo wa mfumo wa fedha za Kiislamu, kwa kuwezesha taasisi na watu binafsi kuwekeza, kupata mapato halali na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi. Juma aliishukuru Wizara ya Fedha na Mipango kwa kusimamia ipasavyo utekelezaji wa mpango huo, akisema umefanikiwa kama ulivyopangwa na kuleta matokeo chanya katika soko la fedha. Alibainisha kuwa mfumo wa Sukuk unatumiwa na mataifa mbalimbali duniani kufadhili miradi mikubwa ya maendeleo, na si nchi za Kiislamu pekee. Alitolea mfano nchi kama United Kingdom na Belgium, ambazo pia zimetumia mfumo huo kama chanzo mbadala cha fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Zanzibar Sukuk1 Limited, Masoud Rashid Mohamed, alisema taasisi hiyo imeanzishwa mahsusi kusimamia miamala ya Sukuk kwa mujibu wa sheria za Kiislamu, kuanzia hatua ya utoaji (issuance) hadi usimamizi wake. Alisema tayari taasisi hiyo imeanza kutoa gawio la awali kwa wawekezaji na kufanya tathmini ya utekelezaji wake ili kubaini changamoto na kuzitatua mapema. Aidha, katika bajeti ya mwaka huu, wamepanga kuanzisha mfumo wa kidijitali utakaorahisisha uendeshaji wa miamala hiyo, ambapo unatarajiwa kuanza kufanya kazi rasmi katika robo inayofuata ya mwaka wa fedha. Masoud alieleza kuwa taasisi mbalimbali za Serikali zimeonesha nia ya kutumia mfumo wa Sukuk kufadhili miradi yao ya maendeleo, ikiwemo Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO), kwa lengo la kutatua changamoto za upatikanaji wa umeme visiwani humo. Naye Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Juma Ali Malik, ameahidi kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo ili kuhakikisha mfumo wa Sukuk unakuwa endelevu na unachangia kikamilifu maendeleo ya Zanzibar. Waziri Malik alisema kuanzishwa kwa Zanzibar Sukuk1 Limited ni hatua ya kimkakati inayolenga kupanua wigo wa vyanzo vya mapato ya Serikali bila kuongeza mzigo wa mikopo yenye riba. Alibainisha kuwa kupitia Sukuk, Serikali itaweza kufadhili miradi ya kimkakati ya miundombinu, nishati na huduma za jamii kwa njia inayokubalika kisheria na kidini. Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kisheria na kiudhibiti ili kuimarisha zaidi soko la fedha za Kiislamu, akisisitiza kuwa dhamira ya Zanzibar ni kujijenga kama kitovu cha huduma za kifedha zinazozingatia misingi ya Sharia katika ukanda huu.

Uncategorized

Serikali Yazitaka Taasisi za Umma Ziwajibike

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Juma Malik Akil amesema mashirika ya umma yanawajibu wa kuisaidia na kuichangia Serikali kupitia gawio na mapato mengine, Dk. Akil aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea Mashirika yanayosimamiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa lengo la kuangalia mwenendo wa Mashirika hayo na kupokea maoni Kwa wakuu mashirika Alisema mashirika mengi hayafanyi vizuri na yameshindwa kujiendesha, hali inayopelekea  kuwa mzigo kwa Serikali, Aliwataka watendaji wa taasisi hizo kutimiza wajibu wao kwa kuwa Serikali imewaamini na kuwapa dhamana ya kusimamia rasilimali za umma kwa manufaa ya taifa. Alieleza kuwa mapato ya Serikali bado hayaridhishi, hususan mapato yasiyo ya kodi, ambayo kwa muda mrefu hayajafanya vizuri licha ya kutegemewa kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na mashirika ya umma. Aidha, alisema wizara hiyo imepewa jukumu la kuyatambua na Mashirika  yanayoleta faida na yale yasiyoleta faida ili kuishauri Serikali hatua stahiki za kuchukua. Aliongeza kuwa katika mwaka ujao wa fedha, Wizara itaanzisha mikataba ya utendaji kati ya ngazi mbalimbali za Serikali ili kupima ufanisi na uwajibikaji wa taasisi hizo. Kuhusu bajeti, Dk. Akil alisema takribani shilingi bilioni 5 na milioni tano zinatarajiwa kutumika katika kuendesha shughuli za kawaida na kugharamia maeneo mengine ya kipaumbele katika mwaka wa fedha ujao. Kwa upande wake, Naibu Waziri wa wizara hiyo, Hamad Omar Bakar, aliwataka watendaji kuanza mara moja kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Waziri ili kufanikisha malengo ya ziara hiyo. Akizungumza katika ziara hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Zanzibar, Mhandisi Shakuru Awadh Suleiman, alisema shirika hilo linajitegemea kwa asilimia 100 huku lieleza kuwa miongoni mwa huduma wanazotoa ni intaneti kwa Serikali kwa bei ya jumla, pamoja na uuzaji wa ‘capacity’ kutoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar, ambapo kwa sasa wana mikonga mitatu ya intaneti. Alisema shirika limejifunza kutoka kwa nchi nyingine zilizofanikiwa kiuchumi kwa kuwekeza katika sekta mahsusi, akieleza kuwa pamoja na Zanzibar kutegemea uchumi wa karafuu, viungo na utalii, sekta ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) ina nafasi kubwa ya kukuza uchumi wa kisasa. Naye Mkurugenzi wa Shirika la Bandari, Akif Ali Khamis, alisema ukuaji wa uchumi unatarajiwa kuongezeka kwa kiasi kikubwa baada ya kukamilika kwa ujenzi wa Bandari ya Mangapwani na bandari nyingine zinazoendelea kujengwa Unguja na Pemba. Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba (ZIC), Sultan Said Suleiman, alisema shirika limejipanga kuisaidia Serikali kupitia miradi ya ujenzi wa nyumba huku akieleza kuwa tayari wamekamilisha na kuuza baadhi ya nyumba, huku wakitarajia kujenga zaidi ya nyumba 4,000 katika miradi ijayo. Aliongeza kuwa wameandaa utaratibu wa kujenga nyumba za gharama nafuu kwa ajili ya kuwakodisha wafanyakazi, hatua inayolenga kuwasaidia kupanga bajeti zao na kuimarisha ustawi wao. Naye Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme Zanzibar, Mhandisi Haji Mohamed Haji, alisema shirika linakabiliwa na changamoto ya miundombinu chakavu na mrundikano wa madeni, hali inayolikwamisha katika utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo. Ziara hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha usimamizi wa BB mashirika ya umma na kuongeza mchango wake katika kukuza mapato ya taifa.

Latest Events

ZIAAT Yatakiwa Kudhibiti Uadilifu wa Taaluma ya Uhasibu

ZIAAT Yatakiwa Kudhibiti Uadilifu wa Taaluma ya Uhasibu Waziri Fedha na Mipango Dkt Juma Malik Akil ameilekeza Bodi ya Wahasibu na Wakaguzi wawashauri elekezi Zanzibar (ZIAAT)kusimamia Kwa karibu maadili na uwajibikaji WA Wahasibu ili kuondoa taswira hasi iliyoibuka Katika jamii kuhusu uaminifu wa Wahasibu Katika matumizi ya Fedha za Taasisi za Umma na Binafsi. Dkt Juma aliyasema hayo wakati wa Ziara yake ya kutemblea ofisi zilizo chini ya Wizara yake.Amesema kumekuwepo na mitazamo mbalimbali mingoni mwa wananchi kuhusu taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi WA Fedha za Umma Hali inayosababiswa na baadhi ya Wahasibu wasikuwa wadilifu walikosa uzalendo na misingi ya maadili na kufanya Kazi kinyume na maadili ya taaluma yao. Amesisitiza kuwa bodi hiyo inawajibikubwa wakusimamia ipasavyo uwadilifu na uwajibikaji WA taaluma hiyo ili kurejesha Imani ndani ya jamii akileza kuwa kazinya Uhasibu na Ukaguzi inahitaji kufwa Kwa kuzingtoa misingi ya Sera Sheria na taratibu zilizopo.

Latest Events

Serikali Yaitaka ZHSF Kuimarisha Uendelevu wa Kifedha

Serikali Yaitaka ZHSF Kuimarisha Uendelevu wa Kifedha WIZARA ya Fedha na Mipango Zanzibar, imeutaka Mfuko wa Huduma za Afya Zanzibar (ZHSF) kuhakikisha unaendelea kuwawezesha wananchi kupata huduma bora za afya huku ukidumisha uendelevu wa kifedha wa mfuko huo. Agizo hilo limetolewa na Waziri wa Wizara hiyo Dk.Juma Malik Akil wakati alipokutana na Bodi ya Wakurugenzi pamoja na watendaji wa mfuko huo, katika ziara yake ya kujitambulisha katika ofisi za mfuko huo Michenzani Moll. Alisema ni muhimu kwa mfuko kujipanga kikamilifu ili kuendelea kuwa endelevu (sustainable) kwani mifuko inayotoa huduma za kijamii mara nyingi hukumbwa na changamoto ya kupoteza uendelevu kutokana na ugumu wa kupima faida za huduma hizo. Aidha alisema uendelevu wa mfuko ni nguzo muhimu katika kuhakikisha huduma za afya zinaendelea kutolewa kwa wananchi bila kuyumba. “Ni muhimu kujipanga vizuri ili mfuko uwe endelevu, kwani hilo litahakikisha huduma zinaendelea kutolewa kwa uhakika na kwa muda mrefu,” alisema. Dk.Juma alibainisha kuwa bado hana uhakika kama mfuko unaweza kuingia kwenye uwekezaji mkubwa kutokana na hatari (risk factors) zilizopo, hivyo alisisitiza fedha zinazopatikana zielekezwe kwenye miradi yenye tija na usalama zaidi. Hata hivyo, alisema serikali imefanya maboresho ya mfumo wa ukusanyaji wa fedha za wanachama, pamoja na kuandaa utaratibu maalum wa kushirikisha wadau mbalimbali ili kuongeza mapato ya mfuko, ambapo kwa awamu ya mwanzo umeanza kwa kuhusisha bima ya wasafiri. Aliahidi kwamba serikali itaendelea kutafuta watu ambao wataweza kusaidia mfuko ili kuongeza uwezo. Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha na Mipango, Hamad Omar, aliutaka mfuko huo kuhakikisha unasimamia kikamilifu sheria na kanuni zake, hususan kwa wananchi wanaojihusisha na vitendo vya udanganyifu katika matumizi ya huduma za mfuko. Alisema yapo malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu utoaji wa huduma pamoja na kutokuelewa mipaka ya huduma zinazotolewa na mfuko huo hivyo aliusisitiza mfuko kuimarisha utoaji wa elimu kwa umma ili wananchi wawe na uelewa sahihi wa mfuko na haki zao. Aliwataka watendaji wa mfuko kutanguliza misingi ya uadilifu, uzalendo na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku ili lengo la kuanzishwa mfuko huo liweze kufikiwa Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Huduma za Afya Zanzibar, Mbarouk Omar Mohammed, aliipongeza serikali kwa kuipa kipaumbele sekta ya afya kwani kuanzishwa kwa mfuko huo kumesaidia kuwapa wananchi uwezo wa kupata huduma za matibabu kwa urahisi zaidi. Alifahamisha kuwa hadi sasa mfuko umefanikiwa kusajili takribani asilimia 50 ya walengwa, huku asilimia nyingine ikiwa bado haijafikiwa, hususan kundi la wastaafu ambao wengi wao bado wako nje ya mfumo wa kupata mafao ya afya. Alisema bodi inaendelea kuchukua hatua kuhakikisha kundi hilo halibaki nyuma na kuiomba serikali kupitia wizara husika kulifanyia kazi suala hilo ili wastaafu nao waweze kunufaika na huduma za afya kupitia mfuko huo. Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji wa ZHSF, Khalifa Muumin Hilal, alisema mfuko huo unaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali wakati wa kuanzishwa kwake. Alieleza kuwa ZHSF imeanzishwa kwa mujibu wa sheria Namba 1 ya mwaka 2023, ikiwa na lengo la kuwa mfuko imara wa kuwawezesha wananchi wote kupata huduma za afya kwa uhakika. Aliongeza kuwa mpango wa mfuko ni kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi kwa kufungua ofisi 11 katika maeneo mbalimbali ikiwemo Tumbatu, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma na ukusanyaji wa michango ya wanachama. Alifahamisha kuwa katika kipindi cha miaka miwili na nusu, mfuko ulilenga kusajili zaidi ya wanachama milioni moja (1,000,000), ambapo hadi Desemba mwaka jana, jumla ya wanachama 999,111 walikuwa tayari wameshasajiliwa. Kwa upande wa michango, alisema mfuko ulilenga kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 1.4, lakini hadi sasa umefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 111. Hata hivyo, alibainisha kuwa mfuko unakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo maslahi ya watendaji, matumizi mabaya ya kadi za wanachama, michango ya wastaafu, upatikanaji wa huduma za afya kwa wote, pamoja na changamoto ya ofisi kwani kwa sasa mfuko unatumia jengo la kukodi. Alisema licha ya changamoto hizo, mfuko unaendelea kuimarisha mifumo yake ya kazi, kusajili vituo vya kutolea huduma na kutoa elimu kwa umma juu ya umuhimu wa kuwa na bima ya afya. Aliongeza kuwa hadi sasa jumla ya vituo vya afya 135 vimeshasajiliwa kutoa huduma kwa wanachama wa Mfuko wa Huduma za Afya Zanzibar na hata kwa Tanzania bara.

Latest Events

BOT Yasihiwa Kuimarisha Uchumi wa Kidijitali Zanzibar

BOT Yasihiwa Kuimarisha Uchumi wa Kidijitali SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema nchi inategemea kwa kiasi kikubwa ukusanyaji wa mapato ya ndani hususan yatokanayo na kodi, ambayo hutumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa manufaa ya wananchi. WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Juma Malik Akil, aliyasema hayo wakati akizungumza na watendaji wa Benki Kuu ya Tanzania Ofisi ya Zanzibar  mara baada ya kufanya ziara ya kutembelea makao makuu ndogo Kinazini. Alisema mapato hayo ni mhimili muhimu katika uendeshaji wa shughuli za serikali na utekelezaji wa mipango ya maendeleo. Dk. Juma alisema tafiti zilizofanywa na wataalamu kutoka Tume ya Mipango zimebaini kuwa Zanzibar inapoteza zaidi ya asilimia 83 ya mapato ambayo ingeweza kuyakusanya endapo kungekuwa na mifumo imara na ya kisasa ya ukusanyaji wa mapato. Alibainisha kuwa upungufu huo unatokana na kutokuwepo kwa mifumo ya kielektroniki katika ukusanyaji wa mapato, hali inayosababisha serikali kukusanya takribani asilimia 17 tu ya uwezo wake halisi. Aidha alisema endapo mifumo ya kidijitali itatumika kikamilifu, kuna uwezekano mkubwa wa kufikia asilimia 100 ya makusanyo, hivyo kuziba pengo la upotevu wa mapato unaofikia asilimia 83 ambayo kwa sasa nchi inashindwa kuyakusanya na nchi inapoteza mapato yake. Akizungumza kuhusu umuhimu wa uchumi wa kidijitali, alisema ni lazima sekta ya fedha ihakikishe kila senti inayopaswa kukusanywa inakusanywa ipasavyo na kuelekezwa katika malengo yaliyokusudiwa, yakiwemo utekelezaji wa miradi ya maendeleo na matumizi ya kawaida ya serikali ili kuleta tija kwa wananchi wanaoitegemea serikali yao. Alibainisha kuwa matumizi sahihi ya mifumo ya kidijitali yataiwezesha nchi kujenga miradi mikubwa ya maendeleo bila kutegemea kwa kiasi kikubwa mikopo. “Nchi inaweza kujenga miradi yake mikubwa bila ya kukopa fedha nyingi hivyo  BOT  endeleeni kutoa elimu kwa wananchi juu ya namna gani ya kutumia mifumo ya kisasa ya kifedha  ili kudhibiti upotevu wa mapato ya serikali,” alisema Dk. Juma alisisitiza kuwa ni lazima nchi iendelee kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo hususan ile ya kimkakati, akibainisha kuwa mapato ya ndani yakikusanywa ipasavyo yatakuwa chachu ya maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi kwa ujumla. Dk.Juma aliitaka BOT kuendelea kushirikiana kwa karibu na sekta mbalimbali za uchumi pamoja na taasisi za utafiti ili kufanya tafiti zenye tija zitakazosaidia kubaini fursa, changamoto na mikakati bora ya kukuza uchumi wa nchi. Alisema tafiti hizo ni nguzo muhimu katika kutoa mwelekeo sahihi wa sera za fedha na maendeleo kwa ujumla. Alisisitiza kuwa tafiti zinazozingatia hali halisi ya uchumi zitasaidia pia kuimarisha uthabiti wa kifedha na kudhibiti changamoto za mabadiliko ya soko la ndani na kimataifa. Aliongeza kuwa serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za Benki Kuu katika kuimarisha tafiti na ukusanyaji wa takwimu sahihi ili kuweka mazingira wezeshi ya maendeleo ya kiuchumi kwani kufanya hivyo  nchi itaendelea kujenga uchumi imara. Alisema serikali imeunda Wizara ya  Mawasiliano Teknologia na Ubunifu ambayo imepewa jukumu mama la  kuhakikisha uchumi wa kidijitali unatumika ipasavyo. Aliipongeza BOT kwa kazi nzuri wanayoifanya kwani mchango wao ni mkubwa kwa serikali hivyo uzalendo , uaminifu na uadilifu ndio msingi imara wa kuendeleza kukuza uchumi wa nchi. Akitoa taarifa ya utendaji wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT), Mkurugenzi wa benki hiyo Ofisi ya Zanzibar Ibrahim Joseph Malogoi alisema benki kuu kimsingi jukumu lake ni kutekeleza kazi za msingi za nenki kuu ya Tanzania. Hata hivyo alisema Benki Kuu inaendelea kutekeleza jukumu lake la msingi kama mhifadhi na mlipaji mkuu wa SMZ na taasisi nyengine za SMT zinazofanya shughuli zake Zanzibar. “Katika kutimiza wajibu huu benki kuu imeendelea kuhakikisha usimamizi thabiti wa akaunti za serikali, uratibu wa miamala yote ya kifedha na utoaji wa huduma za kibenki kwa wakati na ufanisi,” alisema Hata hivyo, alisema hadi Disemba 2025 idadi ya benki za biasjara zinazofanya kazi Zanzibar ni 15 zenye mtandao wa matawi 43. Mkurugenzi Ibrahim alibainisha kuwa makao makuu ndogo ya BOT inaendelea kuhifadhi fedha za SMZ zinazotokana na kodi na zisizotokana na kodi na kuipatia serikali hali halisi ya kifedha kila siku ili iweze kufahya maamuzi sahihi na kuhifadhi, kutoa na kusambaza fedha kwa benki za biashara zilizopo Unguja na kusimamia shughuli za uendeshaji wa kituo cha usambazaji wa noti na sarafu kilichopo Pemba ili kuhakikisha kuwa kuna fedha za kutosha katika mzunguko kwa ajili ya matumizi mbalimbali. Majukumu mengine alisema ni kuhaulisha fedha na kutoa vitabu vya hundi kwa wizara na idaea mbalimbali za SMZ , kuchambua fedha ili kuzirudisja kwenye mzunguko wa fedha zilizo safi na kuziondoa kwenye mzunguko zile zilizochakaa na kutoa elimu kwa wananchi namna ya kuzitambua alama za usalama za noti zao, utunzaji bora wa noti na sarafu na kuhimiza matumizi ya mifumo mengine ya malipo. Sambamba na hayo benki pia inafatilia mwenendo wa uchumi wa Zanzibar kwa kufanya uchambuzi ikiwemo uzalishaji, mwenendo wa mapato na matumizi ya serikali, maendeleo ya sekta ya nje, mwenendo wa deni la serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na maendeleo ya sekta ya fedha. Alifahamisha kuwa benki pia hufanya tafiti mbalimbali ikiwemo utafiti wa hali ya uwekezaji Zanzibar, itafiti wa sekta ya utalii, utafiti wa upatikanaji wa chakula na tafiti nyengine. Alisema katika mwaka huu wa fedha shughuli za miradi mbslimbsli ilipangwa kutekelezwa ambapo hadi kufikia Disemba mwaka 2025 benki kuu Zanzibar imeendelea kutimiza jukumu lakw la kusambaza fedha (noti na sarafu) ili kutosheleza mahitaji ya uchumi bila kusababisha mabadiliko ya kasi ya upandaji wa bei ya bidhaa na huduma. Alisema katika kipindi cha Julai hadi Disemba 2025 benki kuu ilisambaza jumla ya shilingi bilioni 465.6 kati ya fedha hizo bilioni 394.3 zilisambazwa kupitia ofisi ya Unguja na shilingi bilioni 71.3 kupitia kituo cha Pemba. Alisema pamoja na mafanikio hayo zipo baadhi ya changamoto wanazokabiliana nazo ambazo ni pamoja  wananchi kutokuwa na uelewa mzuri kuhusu majukumu ya Benki Kuu ya Tanzania, kutokuwa na uelewa wa fersa za uwekezaji katika masomo ya kifedha, kutokuwa na uelewa wa kutosha wa kuzitambua noti halali na namna bora ya utunzaji wa fedha. Alisema ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya BOT una mchango mkubwa katika kuimarisha sekta ya fedha na kuleta utulivu wa kiuchumi.

Latest Events

Serikali Yaendelea na Mageuzi ya Bajeti na Usimamizi wa Fedha

Serikali Yaendelea na Mageuzi ya Bajeti na Usimamizi wa Fedha WAZIRI wa Fedha na Mipango Zanzibar Dk.Juma Malik Akil, ameiomba kamati ya Bajeti na Kamati ya Kuchunguza na Kudhibiti Hisabu za Serikali (PAC) kuwa karibu na wizara ya fedha katika kuvilinda na kuvitetea vipaumbele ambavyo vitapendekezwa na serikali na baraza liweze kuvibariki. Dk.Juma aliyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku mbili kwa wajumbe wa kamati hizo katika ukumbi wa Dk.Shein ZURA Maisara yaliyoandaliwa na Ofisi ya Mhasibu Mkuu wa serikali. Alisema serikali imepita katika mageuzi makubwa katika miaka mitano na haijasita kwani inahamu kufanya mageuzi makubwa zaidi hasa kuleta maendeleo kwa wananchi wake. Aidha alisema katika kufanya hivyo wanaweza kuwa na mabadiliko katika utekengezaji wa bajeti zake kwani mwaka jana waliweza kufanya bajeti takriban trillion 6.9 ikiwa ni tofauti na bajeti za miaka mitano iliyopita. Alisema ndani ya bajeti hiyo pia waliweka vipaumbele hasa ambapo sehemu kubwa ya vipaumbele hivyo ni utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambapo mwaka jana wametekeleza kwa asilimia 63 ya bajeti nzima ukilinganisha na asilimia 37 ya kazi za kawaida za kila siku. ” Mnaweza kuona jinsi miradi ya maendeleo inavyoonekana wazi kwa kutumia mfumo huu wa kutoa kipaumbele katika bajeti zetu za serikali za miradi ya maendeleo,” alisema Alisema mwaka huu pia serikali ina vipaumbele vyake na tayari wameshaanza michakato wa kuvitengeneza kwa kipindi cha bajeti ya 2026/2027 na miaka mitano ijayo ambayo sehemu kubwa ni kutekeleza ilani ya CCM ya 2015/2030. Alisema pia serikali ina mkakati maalum katika kukusanya mapato kwani ndio roho ya serikali na bajeti ni mapato na matumizi na mara nyingi wamekuwa wakilenga zaidi kwenye matumizi. Waziri Malik alibainisha kuwa wanatamani kupitia kamati kuibua mbinu mpya za mapato kwani serikali imekuwa ikipoteza mapato mengi kutokana na njia zilizoeleka. “Mtusaidie tufanye nini ili kuepuka upotevu huu wa mapato na kushindwa kukusanya kwa sababu mbalimbali ambazo nyengine inawezekana kama tutaweza kuzisimamia vizuri zaidi,” alisema. Alisema serikali hivi sasa inafanya mageuzi kutoka katika mfumo wa fedha taslim (Cash Base) na kutumia mfumo wa kielektroniki lengo ni kuimarisha utendaji baada ya kuona kasoro ambazo zilijitokeza katika mfumo uliopita hasa katika utambuzi wa mali za serikali na ahadi za kifedha zinazowekwa hazipati nafasi kuonekana wazi wazi wakati walipokuwa wakitumia. Alifahamisha kuwa lengo la kuhama huko na kwenda kwenye ‘Acruare Base Aproch’ ni kuhakikisha hayo yote yanapatikana na kwenda sambamba na taratibu za kidunia. Alisema ni matumaini yake kwamba wakipatiwa mafunzo wataweza kuyachukua na kuweza kuwasimamia vizuri zaidi katika utekelezaji wake. “Utekelezaji wa shughuli zetu za kila siku wizara inategemea sana msaada wa kamati zetu hizi mbili kwani zinagusa mnasaba wa utekelezaji wa majukumu yetu,” alisema. Hata hivyo, alisema siku za nyuma ipo mifano ambayo wanatafutiana katika mambo fulani kutokana na kukosa uelewa lakini anaamini watazungumza lugha moja hasa wakati wa kutengeneza bajeti, kutekeleza bajeti na hata kutathimini bajeti watakuwa pamoja na wizara kusaidia kujenga hoja ili watakapowasilisha bajeti zao wawe na wenzao ambao wanawasaidia ndani ya baraza. Dk. Juma akiizungumzia kamati ya PAC alisema wizara inapata changamoto wakati wanapopata ripoti za CAG hivyo ni matumiani yake kamati hiyo itaweza kuwasaidia mapema ili kusiwe na kasoro ambazo zinajitokeza. Alisema kamati hizo zina umuhimu mkubwa kwani zingusa moja kwa moja utendaji wa ofisi yao hivyo alizipongeza kamati hizo kwa kukubali kupokea mafunzo na kushiriki kikamilifu. Naye Mhasibu Mkuu wa Serikali, Hamad Saleh Hamad, alisema mafunzo hayo yamelenga kutoa uelewa kwa kamati hizo juu ya sheria ya fedha ya usimamizi wa fedha za umma ya mwaka 2016. Alisema sheria hiyo ina mambo mengi lakini wameona wajikite katika maeneo matatu ambayo ni muhimu hasa usimamizi wa fedha za umma,usimamizi wa matumizi na matumizi ya viwango kwa taasisi za umma. Haya ni mambo ya msingi na yanahitaji upekee kwa wajumbe wa kamati hizi kuweza kuelewa lakini pia usimamizi wa fedha kwani ndio msingi mkuu wa matumizi ya serikali lakini pia kufuata viwango vya kimataifa kwani hilo ni takwa la kisheria. Katika mafunzo hayo mada mbalimbali ikiwemo usimamizi wa matumizi katika sekta za umma na usimamizi wa fedha za umma kutoka kwenye mfumo wa fedha taslim na kutumia mfumo wa kielektoniki.

Latest News, News

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe.Dkt Juma Malik Akil amewasitiza wastaafu watarajiwa kutumia vizuri mafao ya kustaafu katika uwekezaji sahihi ili kuhimili maisha kipindi cha uzeeni

  Waziri wa Fedha na Mipango Mhe.Dkt Juma Malik Akil amewasitiza wastaafu watarajiwa kutumia vizuri mafao ya kustaafu katika uwekezaji sahihi ili kuhimili maisha kipindi cha uzeeni Ambapo anazitaja kuwa ni jitihada za serikali katika kuwajali wastaafu na kuimarisha mfuko huo ili uendelee kuleta tija katika jamii Tukio hili linaanza uzinduzi wa kitabu cha safari ya ustaafu ambapo ni dira ya kuwaongoza na kutafakari katika maisha yao baada ya kustaafu Mara baada ya tukio hilo Dkt Akil anazungumza na wastaafu watarajiwa katika mafunzo ya maandalizi ya kustaafu kwa wastaafu watarajiwa watakaolipwa na mfuko wa hifadhi ya jamii Zanzibar katika ukumbi wa zssf Michenzani Mall anasema wastaafu wawe watulivu wajiandae na maisha mapya baada ya kustaafu kwao Nae Mkurugenzi Mwendeshaji wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar Ndg. Nassor Shaaban Ameir anasema mafunzo hayo yataleta chachu ya kuwaondolea hofu wastaafu juu ya matumizi sahihi ya mafao hayo ili kuendelea kujiinua kiuchumi Nao Wastaafu watarajiwa wamesema watakuwa makini na ushauri juu ya matumizi ya fedha zao za kustaafu

Scroll to Top