Serikali ya Mapinduzi Zanzibar

wizara ya Fedha na Mipango

Uncategorized

Uncategorized

Mkutano wa Pili wa Mwaka wa Maafisa Ununuzi Zanzibar, 2026

WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Juma Malik Akil, amewataka maafisa manunuzi wa umma nchini kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, uzalendo kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ili kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa ufanisi na kuleta tija kwa taifa. Dk. Malik aliyasema hayo wakati akifungua mkutano wa Pili wa mwaka wa maafisa Ununuzi wa Umma Zanzibar katika ukumbi wa Jaji mstaafu Hamid Mahmoud Hamid (ZEC) Maisara Alisema maafisa manunuzi ni nguzo muhimu katika utekelezaji wa shughuli za serikali kutokana na nafasi yao katika kusimamia matumizi ya rasilimali za umma. Aidha alisema kada hiyo inapaswa kutambua wajibu wake wa msingi wa kusimamia sheria za manunuzi na kuhakikisha kila hatua ya mchakato wa ununuzi inafanyika kwa uwazi, uwajibikaji na kwa kuzingatia maslahi ya taifa. Alisisitiza kuwa maafisa hao wanapaswa kutanguliza uzalendo na maslahi ya nchi badala ya maslahi binafsi, huku wakitekeleza majukumu waliyopewa kwa mujibu wa sheria na mikataba ya ajira. Alisema serikali imekuwa ikipokea malalamiko kuhusu mikataba ambayo haitekelezwi ipasavyo au kushindwa kuilinda maslahi ya taifa hivyo aliwasisitiza  umuhimu wa kuandaa mikataba yenye tija na inayotekelezeka. Dk. Akil alisema sekta ya manunuzi ni mhimili mkubwa wa utekelezaji wa shughuli za serikali kwani takribani asilimia 80 ya shughuli za serikali zinategemea huduma za wataalamu wa manunuzi. Akizungumzia mageuzi ya mifumo, alisema serikali imeamua kuondokana na mifumo ya kienyeji kwa kuanzisha mfumo wa kielektroniki wa e-Procurement System (ePROS) ili kuongeza uwazi, ufanisi na uwajibikaji katika manunuzi ya umma. Aliahidi kuwa serikali inaendelea kuithamini kada ya manunuzi kwa kuimarisha mfumo wa kisheria na mamlaka zinazosimamia sekta hiyo, huku mipango ikiendelea ya kuanzisha chombo cha kitaaluma kitakachosajili maafisa wote wa manunuzi nchini. Alisema hatua hiyo itasaidia kuongeza hadhi ya taaluma hiyo, kuimarisha uwajibikaji wa wataalamu na kuhakikisha maslahi yao yanazingatiwa sambamba na wajibu mkubwa walio nao katika kulinda rasilimali za taifa. Alisema ni imani yake mkutano huo utazaa matunda kwa kada hiyo ili kuona Naye Naibu Waziri wa Wizara hiyo Dk.Hamad Omar Fakih, alisema dhamira kubwa ya serikali ni kuhakikisha manunuzi ya umma yanafanyika kwa uwazi na weledi kwani taasisi hiyo ni muhimu kwa serikali. Aliwataka kutanguliza maslahi ya taifa ili kuhakikisha maendeleo ya nchi yaliyokusudiwa yanafikiwa. Kwa upande wake Mkurugenzi wa Huduma za Sheria, Mohammed Fakih Mzee, alisema maofisa hao wana nafasi ya kipekee kuhakikisha fedha ya umma inatumika na inaleta matokeo yaliyousudiwa. Mapema Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa sera za Ununuzi wa Umma Zanzibar, Omar Said Omar, alisema mkutano huo umelenga kuimarisha uwazi wa ununuzi wa umma kwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Alisema ununuzi wa umma ni nyenzo muhimu na kichocheo cha kimkakati kwa maendeleo ya Zanzibar na kukua kwa uchumi. Alibainusha kuwa lengo kuu ni kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati thabit katika utekelezaji  wa majukumu ya kila siku. Alisema malengo mengine ni kuimarisha mifumo ya kielektoriniki na kushirikisha sekta binafsi. Katika mkutano huo mada mbalimbali ziliwasilishwa ni pamoja na madhara ya rushwa kwa watumishi wa umma, changamoto ya mfumo wa kielktoriki wa katika ununuzi wa umma,

Uncategorized

UFUNGUZI WA MASJALA YA ARDHI

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Fedha na Mipango itaendelea kuimarisha sekta ya ardhi kwa kujenga masjala za kisasa zitakazowezesha uhifadhi  kumbukumbu na taarifa za ardhi kwa mfumo wa kidijitali, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa huduma na kupunguza migogoro ya ardhi. Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Juma Malik Akili, Naibu Waziri wa wizara hiyo, Dk. Hamad Bakar, wakati wa uzinduzi wa Masjala ya Ardhi Makunduchi, alisema Serikali imeamua kwa makusudi kuwekeza katika ujenzi wa masjala hizo ili kuimarisha usimamizi wa taarifa za ardhi nchini. Alisema mfumo huo wa kidijitali utawapa wananchi uhakika wa umiliki wa ardhi zao na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Aidha, aliitaka Kamisheni ya Ardhi kuhakikisha inakitumia kituo hicho kama kilivyokusudiwa ili kuimarisha mipango bora, imara na endelevu ya usimamizi wa ardhi. Aliongeza kuwa Wizara ya Fedha na Mipango kupitia Tume ya Mipango inaendelea na ujenzi wa masjala nyingine katika Wilaya ya Chake Chake, Pemba, katika Kijiji cha Pujini. Amesema uhifadhi wa taarifa na nyaraka za ardhi ni muhimu katika kuzuia upotevu wa kumbukumbu na kupunguza migogoro ya ardhi isiyo ya lazima. Amefahamisha kuwa kupitia   mfumo huo utasaidia kuondoa dhuluma zinazoweza kujitokeza katika umiliki wa viwanja, kuiwezesha Serikali kuwa na kumbukumbu sahihi za ardhi, pamoja na kurahisisha shughuli za uhamishaji wa umiliki na utoaji wa hati kwa wananchi na wawekezaji. Akitoa taarifa ya kitaalamu, Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango Zanzibar, Dk. Afua Mohamed, amesema, Serikali kupitia Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi inaendelea kutekeleza sera na mipango mbalimbali inayolenga kuimarisha usimamizi wa ardhi na kuimarisha utoaji wa huduma. Amesema Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi imekuwa ikiandaa mipango mbalimbali ya kuimarisha usimamizi wa ardhi nchini. Hata hivyo, alibainisha kuwa pamoja na mafanikio yaliyopatikana, sekta ya ardhi bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo upotevu wa nyaraka muhimu za ardhi. Amesema Dhamira ya Serikali ya kujenga kituo hiki ni kuimarisha mifumo ya utunzaji wa taarifa na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa ardhi Ameleza kuwa ogezeko la mahitaji ya ardhi mwaka hadi mwaka linaifanya miundombinu hiyo kuwa muhimu, kwani kutokuwepo kwake kungeendelea kusababisha migogoro mingi ya ardhi. Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Mhaza Gharib Juma, alisema masjala hiyo itakuwa hazina muhimu ya taarifa za ardhi ambazo kwa muda mrefu zimekuwa zikikabiliwa na changamoto za uhifadhi. Amesema vituo hivyo vina umuhimu mkubwa kwa kuwa vitatunza taarifa nyeti za taifa, hivyo akaomba viwekwe uzio kwa ajili ya kuimarisha usalama wake. Aidha, alisisitiza kuwa kutotambuliwa kwa ardhi kwa usahihi ndiko kunakochangia kuongezeka kwa migogoro mbalimbali, hususan ya mipaka. Ujenzi wa Masjala ya Ardhi Makunduchi umegharimu jumla ya shilingi milioni 560 hadi kukamilika kwake.

Uncategorized

NYENZO YA BAJETI YAZINDULIWA

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar, imesema kwa kutambua umuhimu wa jinsia na wazee katika maendeleo ya kijamii kwa mwaka wa fedha 2026/2027 imetenga bilioni 449 katika kutekeleza mpango huo.  Waziri wa Fedha na Mipango Dk. Juma Malik Akil aliyasema hayo wakati akizindua nyenzo za bajeti inayozingatia jinsia (GRV) katika ukumbi wa Wazee Sebleni. Alisema hicho ni kiwango kikubwa ambacho kitawezesha kutekeleza jambo hilo kwa ufanisi kwani bajeti ya mwaka 2025/2026 ilitenga shilingi bilioni 70 pekee. Alifahamisha kuwa uzinduzi huo una umuhimu wa kipekee kwani unafanyika wakati Zanzibar inahitimisha utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Jukwaa la Kizazi Chenye Usawa (Generation Equality Forum) wa miaka mitano, 2021–2026. “Uzinduzi huu ni miongoni mwa mafanikio muhimu ya utekelezaji wa ahadi hizo na unaonesha dhamira ya serikali ya kuimarisha usawa wa kijinsia na uwajibikaji wa matumizi ya rasilimali za umma,” alisema. Alisema bajeti ndio nyenzo kuu ya serikali katika kutekeleza sera na mipango ya maendeleo kwani kupitia bajeti, serikali huamua namna rasilimali zitakavyogawiwa na huduma zitakavyotolewa kwa wananchi. Aidha alisema ni muhimu kuhakikisha kuwa maamuzi hayo yanazingatia mahitaji halisi ya wanawake, wanaume, wavulana  na wasichana ili kuwa na maendeleo jumuishi na yenye manufaa kwa wote. Dk. Malik alisema nyenzo hizo zitachangia utekelezaji wa Dira ya Zanzibar 2050, Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar (ZADEP), Sera ya Jinsia ya Zanzibar ya mwaka 20216 na Mpango wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto awamu ya pili wa mwaka 2025/2026– 2030. Waziri Malik alisisitiza kuwa uzinduzi wa vifaa hivyo si mwisho wa safari, bali ni mwanzo wa hatua mpya ya utekelezaji hivyo alizihimiza wizara, Idara na taasisi za serikali, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Baraza la Wawakilishi, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali na wadau wengine kuhakikisha kuwa vifaa hivyo vinatumika kikamilifu katika majukumu yao ya kila siku Alisema sasa kuna wizara tisa ambazo zinatekeleza mpango huo kwa majaribio na anaamini zitaweza kuongezeka ili kufikia katika kutekelekeza ngazi yote ya kitaifa. Aliipongeza UN Women kwa kuendelea kuwa mshirika muhimu wa serikali katika kuimarisha usawa wa kijinsia, uwezeshaji wa wanawake na kuendeleza utawala bora na maendeleo jumuishi, Umoja wa Ulaya (European Union) na Gates Foundation kwa msaada wao wa kifedha uliowezesha maandalizi, mapitio na ukamilishaji wa vifaa hivyo muhimu. Naye, Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Anna Attanas Poul, alisema uzinduzi huo ni hatua muhimu kwani itaimarisha uwezo wa wizara na wadau wake kuhakikisha kuwa masuala ya kijinsia yanazingatiwa kikamilifu katika mipango, bajeti na utekelezaji wa programu za maendeleo. Alisema alisema UN Women kwa kushirikiana na washirika wake wameendelea kuiunga mkono serikali katika kuimarisha Bajeti Inayozingatia Jinsia na usimamizi wa fedha za umma unaozingatia usawa na ujumuishi. Kwa upande wake Mwakilishi wa UN Women Tanzania, Catharine Gifford, alisema bajeti inayozingatia jinsia ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha rasilimali za umma zinawanufaisha wananchi wote kwa usawa bila kujali jinsia. Aliipongeza SMZ kwa juhudi zake za kuingiza masuala ya kijinsia katika mifumo ya mipango na bajeti kwani bajeti inayozingatia jinsia sio bajeti maalumu kwa wanawake au wanaume pekee bali ni mfumo unaolenga kuhakikisha sera, mipango na matumizi ya fedha za umma yanazingatia mahitaji ya wanawake, wanaume, wasichana na wavulana kwa usawa. Alibainisha kuwa mbinu hiyo husaidia kubaini makundi yanayonufaika na matumizi ya umma na yale yanayoweza kubaki nyuma katika mchakato wa maendeleo. Hivyo, aliahidi kuwa UN Women itaendelea kushirikiana na serikali na wadau mbalimbali ili kuhakikisha masuala ya kijinsia yanaingizwa kikamilifu katika upangaji wa mipango, ugawaji wa bajeti na utoaji wa huduma kwa wananchi wote.

Uncategorized

BAJETI YA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO KUWASILISWA

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Juma Malik Akil, amebainisha vipaumbele tisa vya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/2027, vikiwemo kuimarisha usimamizi wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali, kusimamia utekelezaji wa bajeti inayozingatia usawa wa kijinsia pamoja na kupitia sera, sheria, kanuni na miongozo mbalimbali kwa lengo la kuongeza ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma za Serikali. Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwaka wa fedha 2026/2027 katika kikao cha 30 cha Baraza la Wawakilishi kilichofanyika Chukwani, Dkt. Juma amesema wizara hiyo itaendelea kusimamia nidhamu ya matumizi ya fedha za umma, kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato na kuweka mazingira bora yatakayochochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar. Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati ya bajeti ya Baraza la Wawakilishi, Bakari Hamad Bakar, amesema kamati hiyo inashauri wizara kuhakikisha kunakuwepo na matumizi yenye tija ya fedha za umma ili mipango iliyopangwa iweze kutekelezwa kwa ufanisi na kuleta manufaa kwa wananchi pamoja na kukuza uchumi wa nchi. Wakati huo huo, baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliochangia hotuba hiyo wamesisitiza umuhimu wa kuimarishwa kwa ukusanyaji wa mapato ya ndani, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa wakati ili kufikia malengo yaliyokusudiwa. Akijibu hoja za wajumbe, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Juma Malik Akil, amesema Serikali itaendelea kuyafanyia kazi mapendekezo yote yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa bajeti na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Zanzibar. Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliipitisha bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango ya zaidi ya shilingi trilioni nane kwa ajili ya kutekelezav majukumu na vipaumbele vilivyoainishwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Uncategorized

MAKATIBU WAKUU WAKUTANA KOREA

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar Ndugu Aboud Hasan Mwinyi ameongoza ujumbe wa Tanzania katika kikao cha Makatibu Wakuu wa nchi za Afrika na Korea uliofanyika jijini Seoul nchini Korea. Mkutano huo umefanyika tarehe 1 na 2 Juni, 2026.

Uncategorized

MWENYEKITI WA SUKUK APONGEZA SERIKALI

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Zanzibar Sukuk1 Limited, Juma Amour Mohamed, amempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Ali Mwinyi, kwa maono na juhudi zake za kuanzisha mfumo wa hati fungani za Kiislamu (Sukuk), akisema hatua hiyo ni ya kihistoria katika kuimarisha sekta ya fedha visiwani humo.Akizungumza kuhusu mafanikio ya hatua hiyo, Juma alisema Zanzibar inalenga kuwa kitovu cha huduma za fedha za Kiislamu katika ukanda wa Afrika Mashariki. Alieleza kuwa kuanzishwa kwa hati fungani zinazoendeshwa kwa misingi ya Sharia kumejibu kilio cha muda mrefu cha taasisi za fedha za Kiislamu zilizokuwa zikikosa fursa salama za uwekezaji. Alisema kabla ya kuanzishwa kwa Sukuk, benki na taasisi nyingine za kifedha zilizokuwa zikitoa huduma za Kiislamu zilikuwa zikikabiliwa na changamoto ya ukwasi mkubwa (liquidity) bila kuwa na maeneo yanayokubalika kisheria kwa uwekezaji. Hali hiyo ilisababisha kupungua kwa ufanisi wa utendaji katika soko la fedha. “Benki za Kiislamu zilikuwa na fedha nyingi lakini hazikuwa na miradi au dhamana zinazokidhi matakwa ya Sharia kwa ajili ya kuwekeza. Hii iliathiri utendaji wao na hata kuwanyima watu binafsi fursa za uwekezaji halali,” alisema. Aliongeza kuwa kuanza kwa Sukuk kumesaidia kukamilisha mnyororo wa mfumo wa fedha za Kiislamu, kwa kuwezesha taasisi na watu binafsi kuwekeza, kupata mapato halali na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi. Juma aliishukuru Wizara ya Fedha na Mipango kwa kusimamia ipasavyo utekelezaji wa mpango huo, akisema umefanikiwa kama ulivyopangwa na kuleta matokeo chanya katika soko la fedha. Alibainisha kuwa mfumo wa Sukuk unatumiwa na mataifa mbalimbali duniani kufadhili miradi mikubwa ya maendeleo, na si nchi za Kiislamu pekee. Alitolea mfano nchi kama United Kingdom na Belgium, ambazo pia zimetumia mfumo huo kama chanzo mbadala cha fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Zanzibar Sukuk1 Limited, Masoud Rashid Mohamed, alisema taasisi hiyo imeanzishwa mahsusi kusimamia miamala ya Sukuk kwa mujibu wa sheria za Kiislamu, kuanzia hatua ya utoaji (issuance) hadi usimamizi wake. Alisema tayari taasisi hiyo imeanza kutoa gawio la awali kwa wawekezaji na kufanya tathmini ya utekelezaji wake ili kubaini changamoto na kuzitatua mapema. Aidha, katika bajeti ya mwaka huu, wamepanga kuanzisha mfumo wa kidijitali utakaorahisisha uendeshaji wa miamala hiyo, ambapo unatarajiwa kuanza kufanya kazi rasmi katika robo inayofuata ya mwaka wa fedha. Masoud alieleza kuwa taasisi mbalimbali za Serikali zimeonesha nia ya kutumia mfumo wa Sukuk kufadhili miradi yao ya maendeleo, ikiwemo Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO), kwa lengo la kutatua changamoto za upatikanaji wa umeme visiwani humo. Naye Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Juma Ali Malik, ameahidi kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo ili kuhakikisha mfumo wa Sukuk unakuwa endelevu na unachangia kikamilifu maendeleo ya Zanzibar. Waziri Malik alisema kuanzishwa kwa Zanzibar Sukuk1 Limited ni hatua ya kimkakati inayolenga kupanua wigo wa vyanzo vya mapato ya Serikali bila kuongeza mzigo wa mikopo yenye riba. Alibainisha kuwa kupitia Sukuk, Serikali itaweza kufadhili miradi ya kimkakati ya miundombinu, nishati na huduma za jamii kwa njia inayokubalika kisheria na kidini. Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kisheria na kiudhibiti ili kuimarisha zaidi soko la fedha za Kiislamu, akisisitiza kuwa dhamira ya Zanzibar ni kujijenga kama kitovu cha huduma za kifedha zinazozingatia misingi ya Sharia katika ukanda huu.

Uncategorized

Serikali Yazitaka Taasisi za Umma Ziwajibike

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Juma Malik Akil amesema mashirika ya umma yanawajibu wa kuisaidia na kuichangia Serikali kupitia gawio na mapato mengine, Dk. Akil aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea Mashirika yanayosimamiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa lengo la kuangalia mwenendo wa Mashirika hayo na kupokea maoni Kwa wakuu mashirika Alisema mashirika mengi hayafanyi vizuri na yameshindwa kujiendesha, hali inayopelekea  kuwa mzigo kwa Serikali, Aliwataka watendaji wa taasisi hizo kutimiza wajibu wao kwa kuwa Serikali imewaamini na kuwapa dhamana ya kusimamia rasilimali za umma kwa manufaa ya taifa. Alieleza kuwa mapato ya Serikali bado hayaridhishi, hususan mapato yasiyo ya kodi, ambayo kwa muda mrefu hayajafanya vizuri licha ya kutegemewa kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na mashirika ya umma. Aidha, alisema wizara hiyo imepewa jukumu la kuyatambua na Mashirika  yanayoleta faida na yale yasiyoleta faida ili kuishauri Serikali hatua stahiki za kuchukua. Aliongeza kuwa katika mwaka ujao wa fedha, Wizara itaanzisha mikataba ya utendaji kati ya ngazi mbalimbali za Serikali ili kupima ufanisi na uwajibikaji wa taasisi hizo. Kuhusu bajeti, Dk. Akil alisema takribani shilingi bilioni 5 na milioni tano zinatarajiwa kutumika katika kuendesha shughuli za kawaida na kugharamia maeneo mengine ya kipaumbele katika mwaka wa fedha ujao. Kwa upande wake, Naibu Waziri wa wizara hiyo, Hamad Omar Bakar, aliwataka watendaji kuanza mara moja kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Waziri ili kufanikisha malengo ya ziara hiyo. Akizungumza katika ziara hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Zanzibar, Mhandisi Shakuru Awadh Suleiman, alisema shirika hilo linajitegemea kwa asilimia 100 huku lieleza kuwa miongoni mwa huduma wanazotoa ni intaneti kwa Serikali kwa bei ya jumla, pamoja na uuzaji wa ‘capacity’ kutoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar, ambapo kwa sasa wana mikonga mitatu ya intaneti. Alisema shirika limejifunza kutoka kwa nchi nyingine zilizofanikiwa kiuchumi kwa kuwekeza katika sekta mahsusi, akieleza kuwa pamoja na Zanzibar kutegemea uchumi wa karafuu, viungo na utalii, sekta ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) ina nafasi kubwa ya kukuza uchumi wa kisasa. Naye Mkurugenzi wa Shirika la Bandari, Akif Ali Khamis, alisema ukuaji wa uchumi unatarajiwa kuongezeka kwa kiasi kikubwa baada ya kukamilika kwa ujenzi wa Bandari ya Mangapwani na bandari nyingine zinazoendelea kujengwa Unguja na Pemba. Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba (ZIC), Sultan Said Suleiman, alisema shirika limejipanga kuisaidia Serikali kupitia miradi ya ujenzi wa nyumba huku akieleza kuwa tayari wamekamilisha na kuuza baadhi ya nyumba, huku wakitarajia kujenga zaidi ya nyumba 4,000 katika miradi ijayo. Aliongeza kuwa wameandaa utaratibu wa kujenga nyumba za gharama nafuu kwa ajili ya kuwakodisha wafanyakazi, hatua inayolenga kuwasaidia kupanga bajeti zao na kuimarisha ustawi wao. Naye Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme Zanzibar, Mhandisi Haji Mohamed Haji, alisema shirika linakabiliwa na changamoto ya miundombinu chakavu na mrundikano wa madeni, hali inayolikwamisha katika utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo. Ziara hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha usimamizi wa BB mashirika ya umma na kuongeza mchango wake katika kukuza mapato ya taifa.

Scroll to Top